Taifa Tanzania
Taifa Tanzania. Gazeti Huru la Afrika Mashariki linaloandaliwa kwa lugha ya kiswahili

Kesi ya Wanavijiji Loliondo Dhidi ya Pori Tengefu la Pololeti Kusikilizwa Novemba 8

Shauri lililofunguliwa na wananchi watano wa loliondo ya kupinga tangazo la serikali namba 421 la kutangaza kilomita 1500 za mraba kuwa pori tengefu la Pololeti inatarajiwa kuanza kusikilizwa tarehe 8 Novemba, 2022.

Kesi hiyo itakayosikilizwa na jaji Mohamed Gwae wa mahakama kuu kanda ya Arusha ilitajjwa katika mahakama kuu ya Arusha mbele ya mawakili watatu wa serikali pamoja na mawakili sita wa upande wa  utetezi ambao ni wanavijiji kutoka wilayani Loliondo.

Wananchi wa tano wa Wilaya ya liliondo walifungua kesi ya kuiomba mahakama izuie tangazo hilo la serikali na kukosa uhalali, kuondoa zuio hilo la Serikali pia Mahakama itamke kuwa Serikali pamoja na watumishibwake wasiruhusiqe kuwazuia wananchi kufika na kufanya shughuli zao.

Wakizungumza wakati kesi hiyo ilipotajwa Mawakili wa serikali, Peter Mseti, Jackline Kinyasi na Saley Manoro  wameiomba mahakama kuwapa muda wa siku saba ili kuleta viapo kinzani  huku wakieleza mahakama  kuwa kwa sasa eneo hilo limekwishapandishwa hadhi kutoka pori tengefu na kuwa pori la akiba.

Nao baadhi ya Mawakili upande wa utetezi, Alais Melau, Denis Mosses na Yohana Masiaya wamepinga taarifa hiyo ya kupandishwa hadhi kwa eneo hilo kutoka pori tengefu kuwa pori la akiba la Pololeti kwani utaratibu wa awali ni batili na haukushirikisha wananchi kama sheria inavyotaka.

Shauri No 9 ya Mwaka 2022 kuhusu Maombi ya Mapitio ya Sheria (Judicial Review Application) dhidi ya Tangazo la Waziri wa Mali asili na Utalii (GN no 421) ya tarehe 17 Juni 2022kuhusu ardhi ya Vijiji vya Loliondo kuwa Pori Tengefu la Pololeti, limeahirishwa baada ya wajibu maombi kuomba siku Saba ili waweze kuleta majibu.

Mahakama imekubali ombi la Wajibu Maombi yaani Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Maliasili na Utalii na Mahakama imepanga kusikiliza shauri hilo tarehe 8 Novemba ,2022 saa 8:00 Mchana

Katika shauri hilo Waleta maombi Watano kutoka vijiji vilivyoathirika wanaomba Mahakama iagize Serikali kuondoa zuio dhidi ya Wananchi kuingia kwenye eneo la Kilometa za mraba 1500 ambalo wamekuwa wakitumia kwa ajii ya malisho ya mifugo yao na kwa ajili ya kufanyia shughuli za imani yao

Na kwamba Mahakama itamke kwamba Tangazo la Serikali (GN421) la tarehe 17 Juni 2022 ni Batili na lisitumike kwani ni kinyume na sheria na pia haikuwashirikisha wananchi kama sheria inavyotaka

Mahakama itamke kuzuia Serikali na Mawakala wake wasifanye oparesheni zote kwenye eneo hilo